MKURUGENZI WA TANESCO MHANDISI ENG, GISSIMA NYAMO-HANGA AFARIKI DUNIA KWA AJALI BUNDA

TANZIA 

Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Usambazaji Umeme Tanzania (Tanesco), Gissima Nyamo-Hanga amefariki dunia usiku wa kuamkia leo Aprili 13, 2025 katika ajali iliyotokea wilayani Bunda mkoani Mara.

Mkuu wa Mkoa wa Mara, Evans Mtambi amethibitisha kutokea kwa tukio hilo, ambapo amefafanua kuwa  limetokea kati ya saa 6 hadi 7 usiku wa kuamkia leo.

“Ni kweli tukio lipo na amefariki dunia ila wasiliana na RPC atakuwa na taarifa kwa kina,” amesema  Mtambi

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mara, Pius Lutumo amethibitisha kutokea kwa tukio hilo akisema ni baada ya gari la Mkurugenzi lililokuwa likitokea Mwanza kwenda Bunda kugongana uso kwa uso na lori.

Amesema chanzo cha tukio hilo ni dereva wa gari lililokuwa limembeba Mkurugenzi aina ya Toyota Land Cruiser kumkwepa mwendesha baiskeli kisha kupoteza mwelekeo na kugongana na lori.

“Tukio limetokea Bunda saa 7.30 usiku baada ya dereva wa gari aina ya Toyota Land Cruiser iliyombeba mkurugenzi kumkwepa mwendesha baiskeli na kugongana uso kwa uso na lori kisha kupelekea vifo vya dereva na bosi wake,” amesema Kamanda Lutumo

Meneja wa Tanesco Mkoa wa Mara, Nickson Babu amesema mwili wa marehemu umehifadhiwa katika Hospitali Teule ya Wilaya ya Bunda huku wakisubiri taarifa zaidi kuhusu taratibu nyingine.

Unataka kutuma habari? Submit on tuma kwetu kupitia info@kigogomedia.com au WhatsApp 07000000